Mkutano Mkuu wa 14 wa Umoja wa Ukoo wa Kivenule (KAUKI) umefanyika Kijijini Kidamali – Iringa tarehe 21 – 22 Juni 2025. Huu ni mwendelezo wa Mikutano ya KAUKI ambayo imekuwa ikifanyika kila Mwaka katika Kanda zake mbalimbali. Mkutano Mkuu wa 14 wa KAUKI ulijumuisha ndugu na wanaukoo kutoka maeneo ya Kanda mbalimbali za Kidamali, Magubike, Irore, Nduli, Dar es Salaam, Kalenga, Iringa Mjini, Kihesa, Ibogo nk na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa Mjini.
Jumla ya Wanaukoo zaidi ya 100 kutoka Ukoo wa Kivenule waliohudhuria Mkutano Mkuu wa 14 wa KAUKI, wakiwemo watu wazima na watoto.
Mkutano Mkuu wa 14 wa KAUKI kwa mara ya kwanza ulikuwa na uwakilishi mkubwa kutoka Vilalo katika Kanda ya Irore.
Awali ya yote Mtendaji wa Kijiji cha Kidamali Ndugu Raphael Linus alitoa nasaha na baraka zake kwenye Mkutano huo, huku akiwapongeza Wanaukoo wa Kivenule kwa kuwa na Mikutano kama hii.
Mwenyekiti wa Ukoo wa Kivenule ndugu Onesmo Bernard Kivenule aliwaomba wanaukoo kuwa na tabia ya kujibu jumbe mbalimbali zinazotumwa kwa Wanaukoo ili kuongeza ari na hamasa kwa wahamasishaji. Hali kadhalika aliwapongeza Wanaukoo wanaochangia fedha ili kufanikisha Mikutano ya Ukoo. Alienda mbali zaidi kwa kuwapa maua yao Wanaukoo wanaowezesha shughuli za Mikutano kwa kuchangia kiasi kikubwa cha fedha. "Kila anayetoa kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya Mikutano ya KAUKI, hakika huyu ni Mwezeshaji. Michango yao inawainua wale wenye kidogo". Changamoto ambayo bado wanaukoo tunakabiliana nayo ni mwitikio wa Wanaukoo katika Mikutano hii. Pia changamoto ya uchumi duni miongoni mwetu.
Mwenyekiti wa Ukoo wa Kivenule aliongeza kwa kusema kuwa, mojawapo ya mafanikio makubwa ya mikutano hii ni pamoja na wanaukoo kufahamiana na pia kuwajua ndugu toka sehemu mbalimbali.
Umoja wa Ukoo wa Kivenule umekuwa ukiwasaidia ndugu katika changamoto mbalimbali ikiwemo ugonjwa, huku akitolea mfano baadhi ya ndugu waliosaidiwa kwa kiasi Fulani na Wanaukoo baada ya kupata maradhi. Wanaukoo wamekuwa wakishiriki kwa kutoa michango yao ili kuwafanya ndugu zao wapate tiba pale inapobidi.
Pia Mwenyekiti wa KAUKI aliwafahamisha Wanaukoo kuhusu Mpango Madhubuti wa Ukusanyaji wa Michango kwa kutumia M-KOBA kwa lengo la kutoa uhakika wa usalama wa fedha za Wanaukoo na pindi kila aliyechangia kupata taarifa za miamala anayochangia. Mwenyekiti ameendelea kuwahimiza wanaukoo kujiunga na M-Koba ya TAGUMTWA huku akiwasihii wale wanaopata changamoto ya kujiunga kuwasiliana naye.
Mwenyekiti aliwajulisha Wanaukoo kuwa Michango ya KAUKI kwa mwaka kwa ajili ya Mkutano wa KAUKI kiwango cha chini ni 30,000/- ambapo itamwezesha kila Mwanaukoo kushiriki vizuri mkutano kwa kupata huduma zote ikiwemo T-shirt. Japo aliendelea kuwaomba wanaukoo ambao wamekuwa wakiwezesha Mikutano hii kuendelea kufanya hivyo kwa kuchangia kiwango kikubwa kama ilivyofanyika katika Mkutano wa 13 na mkutano huu wa 14.
Mshauri wa Umoja wa Ukoo wa Kivenule Ndugu Faustino Sigatambule Kivenule alibainisha kuhusu changamoto ya ushiriki katika mikutano ya KAUKI. Alisema kuwa mahudhurio siyo mazuri na siyo mabaya. Aliwaonya wanaukoo wanaotaka kutia doa kwenye ukoo. Muda wa kubembelezana umeisha na kuahidi kuwa wanaukoo ambao watakuwa hawapendi kushirikiana na wenzao taarifa zitawasilishwa kwenye Ofisi ya Kijiji cha Kidamali.
Mshauri alisisitiza kuwa kama Wanaukoo tunahitaji kufanya kazi kwa bidii ili kujiletea maendeleo. Tuachane na dhana za wivu na imani za uchawi; badala yake tuongeze mwamko katika kuuchangia ukoo na kufanya kazi. Ukoo umekuwa hauingilia masuala ya kifamilia ili wanaomba kushirikishwa ili kama kuna changamoto ziweze kutatuliwa ili kuendelea kuwa na mahusiano mazuri baina ya wanaukoo.
Mshauri alionya tabia ya Wanaukoo kuuza ardhi au mali nyingine za ukoo. Hii itasaidia sana kupunguza migogoro ya kifamilia miongoni mwa wanaukoo. Ukoo ulishaweka taratibu kuhusu uuzaji wa mali ndani ya maeneo ya ukoo. Ukoo lazima ushirikishwe kikamilifu na hata kama inauzwa kipaumbele iwe ni kwa mwanaukoo na siyo mtu wa nje ya ukoo. Amelaani baadhi ya tabia zinazofanyika kuuza ardhi na viwanja ndani ya ukoo kwa sababu ni hatari na inaweza kusababisha mgawanyiko wa wanaukoo; umoja huu umeundwa kwa gharama kubwa kwa kipindi kirefu na unapaswa kulindwa kwa kudumisha mahusiano bora baina ya familia na wanandugu.
Kwa upande wa Kanda ya Kidamali, Mwenyekiti wa Kanda hiyo Katekista George Sigatambule Kivenule aliwafahamisha wanaukoo kuwa bado kuna changamoto kwa baadhi ya ndugu kutoshiriki katika mikutano ya KAUKI. Baadhi wanajitenga kwa sababu binafsi na kama Ukoo kupitia Kanda ya Kidamali wanaandaa taratibu za kuweza kukabiliana na changamoto hizi, ikiwemo kushirikiana na viongozi wa Kijiji cha Kidamali. Ndugu wanaojitenga na wanaukoo wakipata changamoto mara moja huja kwa wanaukoo kuhitaji msaada. Jambo hili haliwezi kuendelea kuvumiliwa.
Mwenyekiti wa Kanda ya Magubike Ndugu Vitus Nzala alibainisha baadhi ya Changamoto za wanaukoo kuwa na mwitikio mdogo kwenye mikutano, hususani baadhi ya ndugu toka eneo la Ibogo na Ilalasimba. Baadhi ya ndugu wanadharau mikutano hii "Mbedasi" kwa kutokuunga mkono mikutano hii.
Makamu Mwenyekiti wa Kanda ya Irore, Ndugu Nasson Kivenule yeye alibainisha kuwa amejifunza mambo mengi kuhusu Mikutano ya KAUKI kwa sababu kwa wengi wao imekuwa ni mara ya kwanza kushiriki.
Mwakilishi wa Kalenga yeye alibainisha kuwa ushiriki mdogo toka Kalenga unachangiwa na ndugu wa Ukoo wa Matagi kupata msiba.
Wanaukoo wakiwa katika sare (T-shirts) Nyeupe na chache za rangi ya Kahawia, Bluu, Kijivu na Nyeusi walihudhuria na kuupendezesha Mkutano.
Mada ya Chimbuko na Historia ya Ukoo wa Kivenule iliwasilishwa katika Mkutano huo sambamba na mada ya Magonjwa yasiyoambuza kama Shinikizo la Damu na Kisuri.
Hakika Mkutano ulifana sana.
Kulikuwa na USIKU WA KAUKI ambapo wanaukoo walipata fursa ya kubadilishana mawazo kwa kula nyama choma na pia kupata vinywaji. Lengo la usiku huu ilikuwa kuwapa nafasi wanaukoo ya kuweza kufahamiana zaidi wao kwa wao na pia baina ya wanandugu wengine.
Kuna ndugu waliofika siku mbili kabla ya siku ya Mkutano ili kuweza kuyajua mazingira na pia kujifunza namna mikutano ya KAUKI inavyoandaliwa. Hakika mkutano mkuu wa 14 wa KAUKI ulipendeza sana.
Mkutano ulihitimishwa kwa kutangaza tarehe ya Mkutano na Kanda ambapo Mkutano Mkuu wa 15 utafanyika. Hivyo, Mkutano wa 14 wa KAUKI uliazimia kuwa Mkutano Mkuu wa 15 utafanyika tarehe 20 – 21 Juni 2026 katika Kijiji cha Vilalo, Irore – Iringa Vijijini.
Sambamba na kutangaza tarehe ya Mkutano – Wanaukoo kwa KAUKI moja walikubali kubadilisha jina la mikutano hii ya KAUKI. Kwa sasa, siku mbili za Mkutano wa KAUKI zitajulikana kama "TAGUMTWA DAY"
TAGUMTWA DAY itafanyika tarehe 20 – 21 Juni 2026, Vilalo – Irore, Iringa Vijijini – Mkoani Iringa.